UJUMBE KUTOKA KWA CEO WA GLORIOUS CELEBRATION.
Wapendwa katika Bwana na wapenzi wote wa Glorious Celebration (GC), BWANA YESU ASIFIWE!
Kwanza kabisa tunamshukuru MUNGU wetu muumba mbingu na nchi kwa vile
ambavyo amekuwa mwaninifu kwetu, kimblilio na nguvu nyakati zote za
huduma na kuzidi kutupa kibali na kutusimamisha kama Walawi wa zama hizi
kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Hakika nafsi zetu hazitachoka kumhimidi
Bwana wala kuzisahau fadhili zake zote. (Zaburi 103:2).
Pili, kwa niaba ya GC family nzima tunapenda kuchukua fursa hii
kuwashukuru ndugu wapendwa katika KRISTO YESU BWANA wetu na wapenzi wote
wa GC kwa ujumla, kwa upendo, maombi na ushirikiano na saburi
mliyoonyesha kwetu tangu kuanza kwa GC.
Wapendwa, kama mtume Paulo
anaenavyo katika 1 Wakorintho 2:4, nasi pia tunajaribu kuongea pasipo
maneno ya kuvutia na ya hekima sana, bali kwa uthibitisho mwingi na
nguvu ya Roho Mtakatifu kwa kusudi kwamba imani yenu ipate kutegemea
nguvu ya MUNGU, na si hekima wala husuda za binadamu.
Ndugu
wapendwa, kuna mambo kadhaa yamejitokeza hivi karibuni ndani ya GC, na
hatimaye kupelekea baadhi ya wana GC kujiengua na kuanzisha kundi
lingine linaloitwa Glorious Worship Team (GWT). Kama nilivyokwisha
kusema hapo juu, hatutapenda sana kuzungumzia mgawanyiko huo katika
namna ya kushambulia upande fulani, kwani tunafurahia zaidi kuzungumzia
umoja na mshikamano uliopo ndani ya GC ili Kristo na azidi kutukuzwa.
Hii ndio maana juzi tulipokuwa Radio Clouds FM 88.5, tulighairi
kuzungumzia juu ya mgawanyiko huu tofauti na wengi mlivyoomba tufanye
hivyo.
Mbeba maono na mwanzilishi wa GC, baba yetu Bishop Ayoub
Mwakang’ata mara zote amesisitiza kuwa, kusudi kuu la huduma hii ni
kuihubiri injili, na hivyo basi injili izidi kusonga mbele bila kumpa
ibilisi nafasi. Wapendwa, GC tunafurahia kuwa vijana wenzetu waliolelewa
GC leo wamekua na kujulikana na hata wameweza kuanzisha kundi lao,
hivyo ni mtazamo na furaha yetu kuwa kazi ya MUNGU imepanuka.
Mgawanyiko huo ulipotokea GC ilitulia na kutafuta kujua nini kusudi la
MUNGU. Hatimaye iliazimiwa kuongeza safu mpya kuungana na wana GC
waliokataa kusaliti maono ya GC. Tangu Mwanzo hadi Ufunuo, siku zote
MUNGU anao watu na siku zote anajisazia watu watakaomwangukia JEHOVAH no
matter what! Hivyo, tulimwomba MUNGU na hatimaye akajiinulia vyombo
vingine vilivyo tayari kuifanya kazi yake. Kisha tulienda kambini kwa
wiki nzima ili kuutafuta uso wa Mungu, na kumwambia BWANA usitutenge na
uso wako, wala ROHO WAKO MTAKATIFU, usituondolee (Zaburi 51:11).
Tulipokuwa huko tulimlingana BWANA na hatukumwacha BWANA mpaka
alipotubariki. BWANA alisema utukufu wa sasa hautakuwa kama ule wa
kwanza. Baada ya hapo tukauona wigo mpana zaidi wa maono ya GC. Na kwa
sasa GC ina timu kubwa zaidi. Mpaka sasa tayari ina waimbaji 24, yaani
ukijumuisha WAPIGA VYOMBO, WAIMBAJI, AKAPELA, na DANCERS. Na makudi
haya yatajumuika katika shughuli mbalimbali za injili. Yaani, uimbaji,
huduma kwa wagonjwa waliotelekezwa mahospitalini, kutembelea yatima na
baadaye wazee na wajane waliotelekezwa.
Tunamshukuru MUNGU,
hatimaye juzi, Jumapili ya tarehe 07/04/2013 GC nzima iliwekwa wakfu
tayari kwa kuanza kazi rasmi tena. (Matendo ya Mitume 1:8 Lakini
mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa
mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria,
na hata mwisho wa nchi).
Neno moja ambalo tumelitaka kwa BWANA
MWAKA HUU, HATUENDI KUIFANYA KAZI PEKE YETU, BALI TUNAKWENDA KUIFANYA
KAZI PAMOJA NAYE. BILA NGUVU, KIBALI NA UWEPO WAKE KATIKATI YETU
HATUTAENDA! (Kutoka 33:15). KILIO NA MAOMBI YETU NI KUIFANYA KAZI YA
BWANA KUPITA WAKATI WOTE TULIOWAHI, TUNATAKA KUONA MUNGU AKIINULIWA
TANZANIA, AFRIKA NA HATA MIISHO YA NCHI. (Yohana 12:32 Nami nikiinuliwa
juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu.)
Wapendwa, GC ni maono kutoka
kwa MUNGU. GC ilianzia madhabahuni, na hivyo MUNGU aliyeanziisha kazi
hii ndani ya mtumishi wake ndiye atakayeitimiza.
GC iko tayari na kuanzia mwezi ujao tutaanza ziara za mikoani na kwingineko.
CEO,
Glorious Celebration.
No comments:
Post a Comment